Like Us On Facebook
Follow Us on Twitter

Janga Jipya Zito Lawakumba Tena Watumishi Wa Umma Wenye Vyeti Feki


Ni janga lingine jipya kwa watumioshi waliokutwa na vyeti feki. Hivi ndivyo inavyoweza kuelezwa kutokana na kuwapo kwa dalili kuwa wale watumishi wa serikali 9,932 waliobainika kuwa na vyeti feki.
Watumishi hao si tu wako katika tishio la kufungwa jela kwa kosa la kughushi bali pia wanakabiliwa na uwezekano wa kupoteza mafao yote kwa kipindi cha utumishi wao.
Tishio hilo ambalo linaweza pia kuwaathiri katika mchango yao iliyokuwa ikipelekwa kila mwezi katika mifuko mbalimbali ya hifadhi ya jamii na ya pensheni ikiwamo ya NSSF, PDPF, LAPF, na GEPF linatokana na baadhi ya maelezo ya wanasheria na pia wabunge waliozungumza kueleza hatima ya jambo hilo.
Hata hivyo, Waziri wa Nchi Ofisi ys Rais Utumishi na Utawala Bora, Angella Kairuki hakuwa tayari kulizungumzia jambo hilo alipoulizwa jana na kutupa mpira kwa Katibu Mkuu wa Wizara yake, Dk. Laurean Ndumbaro, ili kpata ufafanuzi wa suala hilo.
Juzi, baada ya kupokea ripoti ya uhakiki wa vyeti vya elimu na taaluma vya watumishi wa serikali mjini Dodoma na kubainika kuwa 9,932 walitumia vyeti vya kughushi kupata ajira, Rais Magufuli alisema watu hao ni sawa na wezi na majambazi, hivyo wajiondoe kufikia Mei 15, mwaka huu, kabla hawajafikishwa mahakamani ili wakahukumiwe vifungo vya hadi miaka saba kwa wale watakaokutwa na hatia, kama sheria zinavyoeleza.
Aidha, Rais Magufuli aliuagiza pia watumishi hao wenye vyeti feki wasilipwe mishahara na nafasi zao za kazi zitangazwe ili wenye sifa waombe na kuajiriwa ili wazizibe.
Katika ripoti hiyo iliyokabidhiwa kwa Rais na Waziri Kairuki, ilibainika vilevile kuwa watumishi wa umma 1,538 wamekuwa wakitumia vyeti vinavyofanana taarifa huku wengine 11,596 wakiwa na vyeti visivyokamilika kwa kuwa na vya kitaaluma bila ya kuwa na vyeti vya kidato cha nne na cha sita.
Baadhi ya wabunge na pia wanasheria walitoa maoni tofauti kuhusiana na sakata hilo la vyeti feki, wengine wakisema kuwa wahusika hawana chao tena katika mafao kutokana na kosa la kughushi vyeti vya elimu na kitaaluma kuwakosesha sifa ya kupata mafao hayo.
Akizungumzia suala hilo, wakili kutoka kampuni ya South Law Chamber, Deogratius Mwarabu, alisema watu hao wamepoteza sifa za kupata mafao yao kwa sababu ya kosa la kughushi. Alisema kosa kama hilo linapothibitika mahakamani, mhusika hufungwa kwenda jela miaka saba bila faini, na hiyo ni kwa mujibu wa sheria za nchi.
Sheria hairuhusu suala hilo (la kughushi vyeti)… mtu anapobainika hupoteza sifa na kutakiwa kuchukuliwa sheria ikiwa ni pamoja na kushtakiwa,” alisema Mwarabu.
Hata hivyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, Dk. Hellen Kijo Bisimba, alisema wahusika wanastahili kulipwa mafao yao kwa sababu mfumo mbovu waliokutana nao wakati wanaajiriwa ndiyo uliowawezesha kufanya kazi kwa kipindi chote hicho wakiwa na vyeti vya kughushi.
“Licha ya sheria kukataza jambo hilo, lakini wahusika (waliokutwa na vyeti feki) wanastahili kupata mafao yao kwa sababu walipata ajira kutokana na mfumo mbovu wa serikali uliokuwapo…miongoni mwao wapo ambao wametumikia ajira zao na wanakaribia kustaafu na hivyo walipwe haki zao,” alisema Bisimba.
Alisisitiza kuwa watu hao wametenda kosa la kughushi vyeti lakini na serikali ilijiwekea mfumo mbovu ambao uliruhusu matatizo kama hayo kutendeka.
Katibu wa Shirikisho la Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) Mkoa wa Dodoma, ambaye pia ni Katibu wa RAAWU Kanda ya Kati, Ramadhani Mwendwa, aliitaka serikali ikiri kufanya makosa ya kuwapa ajira wahusika kizembe bila kuhakikisha vyeti vyao na hivyo hakuna sababu ya kuwanyima mafao yao.
Alisema kutokana na serikali kufanya makosa ya kuwaajiri watumishi hao kizembe tangu awali, sasa inatakiwa iwalipe mafao yao kutokana na kazi waliyoifanya kipindi chote wakiwa waajiriwa. “Inawezekana hata watumishi wengine wa umma waliostaafu, walikuwa na vyeti feki lakini mafao walilipwa… hivyo hata hawa waliondolewa kwa kosa hilo wanatakiwa kulipwa kwa kuwa wamelitumikia taifa,’ alisema katibu huyo.
Mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche (Chadema), alisema kughushi vyeti ni kosa kisheria na hilo haliangalii cheo. Akataka wahusika wafikishwe mahakamani ili wapate haki yao na ikibidi, huko itajulikana kama wanastahili kulipwa mafao yao.
“Inawezekana wengine wameonewa na hawajafanya makosa hayo. Hivyo wanatakiwa wapewe nafasi ya kujieleza mahakamani,” alisema Heche.
Mbunge wa Rujifi, Abdallah Mchengerwa, alisema ni mapema sana kuzungumzia suala hilo la mafao kwa kuwa ndiyo kwanza limetolewa maamuzi na Rais baada ya ripoti ya uhakiki kukabidhiwa kwake.
Mbunge wa Malindi, Ally Saleh (CUF), alisema watumishi hao waliobainika kuwa wanatumia vyeti feki kwa mujibu wa sheria hawapaswi kupewa chochote kama mafao yao. Alisema watumishi hao hawapewi stahili yoyote kwa sababu hata kile walichokuwa wanalipwa hakikuwa stahiki na kwamba, kama alivyosema Rais Magufuli, wahusika walikuwa wakimwibia mwajiri.
“Labda Serikali iwaonee huruma, lakini kama watafuata sheria, wanapaswa kufungwa na kutokulipwa chochote kwa sababu walikuwa wanapata stahiki wasiyostahili,” alisema Saleh,
Aliongeza kuwa kwa mujibu wa sheria ya kazi na mahuisiano kazini, mfanyakazi anayefukuzwa kazi kwa kosa la wizi au udanganyifu hastahili kulipwa chochote zaidi ya kupelekwa mahakamani na kushitakiwa.
Mbunge wa Temeke, Abdallah Mtolea, alisema watumishi watakaoondoka wenyewe kabla ya siku aliyoagiza Rais Magufuli, yaani Mei 15, wanastahili kupewa stahiki zao.
Alisema kwa watumishi ambao watakaidi agizo hilo kufikia tarehe iliyotajwa na Rais, hawastahili kupata mafao kwa sababu watakuwa wamekiuka amri halali ya serikali.

Bonyeza HAPA Kudownload Applicationi Ya Mawingu Blog Kwenye Simu Yako Ili Kupata Habari Zetu Haraka

===

Tupe Maoni Yako Hapa Chini
 

Mawingu Blog | Home Of Newz Copyright © 2017