Like Us On Facebook
Follow Us on Twitter

Kamanda Wa Polisi Amlipisha Askari Faini Kwa Kumbambikizia Dereva Kosa


Kamanda wa Polisi cha Usalama Barabarani wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Awadh Haji amemuamuru askari wake kulipa faini ya shilingi 30,000 baada ya kudaiwa kumbambikizia kesi dereva.

Askari huyo aliyejulikana kwa jina moja la Beatrice anadaiwa kufanya kosa hilo kwa dereva wa gazeti la Jamhuri, Leonce Mujumizi.

Kamanda Haji alisema tukio hilo lilitokea juzi katika mataa ya makutano ya barabara za Uhuru na Msimbazi, Kariakoo.

Alisema dereva huyo alikuwa akitokea Mnazi Mmoja kwenda Ilala na alipofika katika taa hizo alisimama kwa kuwa taa nyekundu ilimzuia kuendelea. Ilipowaka taa ya kijani aliendelea na safari yake na baada ya kuvuka na kufika katikati alisimamishwa na askari huyo huku akimweleza kuwa hakufuata ishara yake wakati yeye (askari) ndiye aliyekuwa anaongoza magari.
“Hata hivyo dereva alimweleza askari huyo kuwa hakumuona bali alifuata maelekezo ya taa” alisema kamanda haji.
Alisema kuwa kuliiibuka mvutano kati yake na dereva huyo na mwishowe askari huyo alimwandikia dereva faini ya shilingi 30,000 kwa kosa la kutofuata ishara yake.
Kamanda Haji alisema dereva huyo hakukubaliana na hatua hiyo na kuwa hakupewa fursa ya kujitetea.
Alisema baada ya kusikiliza pande zote, alibaini kuwa askari wake hakufuata taratibu zinazotakiwa pindi anapomkamata dereva hivyo kuamuru alipe faini hiyo.
“Siku zote hata mahakamani lazima mshatakiwa apewe nafasi ya kujitetea ili akubali kosa au la ndipo uamuzi utolewe na jaji au hakimu. Mimi kama kiongozi sipo tayari kuona mtendaji wangu anafanya makosa na kuyafumbia macho. Ni lazima nichukue hatua ili kila mmoja ajue wajibu wa kazi,” alisema Kamanda Haji.
Mhariri Mtendaji wa gazeti la Jamhuri, Dogratus Balile alisema: Tunamshukuru ACP Awadh kwa kutetea na kusimamia haki bila uonevu. Tunaamini WP Beatrice na mkuu wa trafiki kituo cha Msimbazi, Inspekta Bihemo kuanzia sasa watafanya kazi kwa weledi na kutenda haki kwa kila mmoja.

Bonyeza HAPA Kudownload Applicationi Ya Mawingu Blog Kwenye Simu Yako Ili Kupata Habari Zetu Haraka

===

Tupe Maoni Yako Hapa Chini
 

Mawingu Blog | Home Of Newz Copyright © 2017