Like Us On Facebook
Follow Us on Twitter

Meneja Leaders Club apandishwa kizimbani kwa kutotumia mashine za EFD

Meneja Msaidizi wa Viwanja vya Leaders Club, Emmanuel Chacha (40) amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kinondoni kujibu mashtaka mawili, likiwamo la kushindwa kutumia  mashine za kutoa risiti za kielektroniki (EFD).

Akisoma hati ya mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi, Is-Haq Kuppa, wakili kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Wilaya ya Kinondoni, Juliana Ezekiel alidai mshtakiwa alitenda kosa hilo Novemba 5, 2016 katika ofisi za klabu hiyo zilizopo Ada Estate.

Wakili Ezekiel alidai mshtakiwa kwa kukusudia alishindwa kununua na kutumia mashine hiyo akitambua anafanya kosa kinyume na sheria ya kodi.

Ezekiel katika shtaka la pili alidai meneja huyo akiwa mfanyabiashara wa baa na kukodisha ukumbi kwa kukusudia alishindwa kufuata sheria za kodi.

Wakili Ezekiel alidai upelelezi umekamilika hivyo aliiomba Mahakama kupanga tarehe kwa ajili ya kumsomea maelezo ya awali mshtakiwa.

Hakimu Kuppa alisema kwa mujibu wa sheria mashtaka hayo yana dhamana, hivyo alimtaka mshtakiwa kuwa na mdhamini mmoja anayefanya kazi inayotambulika kwa mujibu wa sheria, ambaye atasaini bondi ya maandishi ya Sh5 milioni.

Mshtakiwa alishindwa kutimiza masharti, hivyo alipelekwa mahabusu. Kesi imeahirishwa na itatajwa Mei 19.

Bonyeza HAPA Kudownload Applicationi Ya Mawingu Blog Kwenye Simu Yako Ili Kupata Habari Zetu Haraka

===

Tupe Maoni Yako Hapa Chini
 

Mawingu Blog | Home Of Newz Copyright © 2017