Like Us On Facebook
Follow Us on Twitter

Wanaume Lindi Walalama Kushindwa Kuwatawala Wanawake Zao


Na.Ahmad Mmow,Lindi.
BAADHI ya wanaume  wa kijiji cha Kilolambwani wamelalamika kushindwa kuwatawala wake zao baada ya wanawake kupewa ellimu inayohusu haki zao.

Hayo yamejiri leo katika kijiji hicho wakati wa utambulisho na makabidhiano ya mradi wa USAWA NA JINSIA unaoratibiwa na kusimamiwa kwa ushirikiano baina ya kituo cha msaada wa kisheria kwa wanawake na watoto cha Lindi(LIWOPAC) na shirika la kimataifa la misaada la OXFAM.

Wanaume hao walisema tangu mashirika na asasi za kiraia,ikiwamo LIWOPAC  kutoa  elimu kwa wanawake kuhusu haki zao na watoto tabia za wanawake zimebadilika.Kwa madai kwamba hawatawaliki na hawaongozeki.Badala yake wanataka usawa kinyume cha maagizo ya imani za dini zao.

Mwanaume aliyejitambulisha kwa jina la Farijala Mchop alisema elimu inayotolewa na mashirika hayo inakwenda kinyume na imani dini zao.Huku akitoa wito kwa mashirika na asasi hizo zihamasishe watu wafunge ndoa za serikali ili usawa unaohubiriwa uweze kutimia.
"Tena hata mahari tuwe tunachanga nusu kwa nusu.Haiwezekani niwe naoa lakini tuwe kama tumeoana.Wanawake sasa wanakuwa juu ya wanaume,"alisema Mchopa.

Mwanaume huyo alikwenda mbali zaidi kwa kutoa wito kwa wanaume wenzake  nchini kuanza mchakato wa kuanzisha vyama na mashirika ya kuwatetea.Kwamadai kwamba baadhi ya wanawake wanawadhulumu,kuwatesa na kuwanyanyasa waume zao.Hata hivyo hawana watetezi.

Maelezo ya Mchopa yaliungwa mkono na Ahmad Mnyanga ambae nae alisema ndoa nyingi zimevurugika.Kwamadai kuwa wanawake wanajiona wanaelewa nakutaka kuwa juu ya waume zao.

"Inaonekana kama wanaume wameumbwa kwa ajili ya kuwatesa wanawake.Wakati hiyo nitabia tu ya mtu,lakini wapo wanawake niwakatili sana.Hakuna sababu ya kusaidiwa na mashirika ambayo kipaumbele chake ni kuwatetea akina mama. Sisi wanaume tuanzishe yetu,kwasababu nao utakuwa usawa pia,wanawake na vyama vyao na wanaume tuwe na vyetu,"Mnyanga alikoleza mjadala.

Hata hivyo malalamiko na wito wa wanaume hao haukubaki salama bila ya kupingwa.Kwani mwanamke aliyejitambulisha kwa jina la Zaria Kafati,licha ya kuyashukuru mashirika na asasi hizo kwa kuwajengea uwezo kuzitambua haki zao na kuzidai,alisema chuki na hasira za baadhi ya wanaume kwa mashirika na asasi za kiraia ni kuona mizizi ya ukandamizaji,dhuluma na unyanyasaji dhidi ya wanawake inakatwa.

Kafati aliongeza kusema nijambo la kushangaza kusikia wanaume wanafikiria kuanzisha vyama  vya kuwatetea,wakati wanajua kwamba kundi kubwa linalodhulumiwa na kuonewa  ni wanawake kuliko wanaume."Kama kuunda vyama basi vitakuwa nivya kutetea uonevu,kwasababu wanawake ni waathirika wakubwa wa vitendo vya unyanyasaji kuliko wanaume,"alisema Kafati.

Kwaupande wake msimamizi wa mradi huo,Romana Colman,licha ya kueleza lengo la mradi huo,alisema asasi za kiraia ikiwamo LIWOPAC hazina nia ya kuzifarakanisha jamii.Bali haki na usawa ndio msingi wa amani na utulivu katika jamii husika.

Ndicho kinachohubiriwa na asasi hizo. "Lakini hata imani za dini za kweli hazijaagiza jinsia fulani idhulumu jinsia nyingine.Bali zimeagiza kutendea wema,haki na usawa.Ndicho ambacho sisi tunaelimisha.Kwakuwa wanaume ndio wanojiona ni viongozi wa wanawake basi  waoneshe mfano wakutenda haki na usawa wa kijinsia.

Mahari ni utaratibu na makubaliano ya wahusika kwenye ndoa kwa mujibu wa ndoa wanazofunga kupitia imani wanazoamini, kwahiyo hakuna sababu ya kuomba mchangishane,"Romana alitoa wito,msisitizo na darasa.

Mradi huo unaofadhiliwa na OXFAM,ambao utakelezwa katika vijiji vya Kilolambwani, Dimba,Pande Ploti na Mikoma Nakimwera,vilivyopo katika wilaya za Lindi na Kilwa, unalengo la kuondoa unyanyasaji katika jamii ili iweze kujikwamua kiuchumi  kutokanana hali ya uchumi iliyopo.

Ambayo inataka kila mtu  awajibike ipasavyo katika nafasi yake ili kujiletea maendeleo.Ambapo mkoani humu (Lindi) utatekelezwa kwa miaka mitano kwa awamu ya miezi sitasita.

Bonyeza HAPA Kudownload Applicationi Ya Mawingu Blog Kwenye Simu Yako Ili Kupata Habari Zetu Haraka

===

Tupe Maoni Yako Hapa Chini
 

Mawingu Blog | Home Of Newz Copyright © 2017